KUENEA KWA KISWAHILI NCHINI RWANDA


1   Sababu Zilizokidunisha Kiswahili Nchini Rwanda Kabla ya Uhuru
Rwanda ni nchi ndogo ya Afrika ya Kati ambapo Kiswahili huzungumzwa kidogo sana. Kwa mujibu wa maelezo ya Maganga (1997:iv) sababu kubwa zilizokifanya Kiswahili kidunishwe na kuzungumzwa au kutumika kidogo sana nchini Rwanda inatokana na historia ya utawala wake wa jadi, kama ifuatavyo:

(a)       Watawala wa jadi hawakukubali watu waliokuwa wakizungumza lugha nyingine waingie na kufanya biashara.

(b)       Biashara kutoka nje ya nchi ilikuwa ikifanywa na makabila ya jirani ambayo yalikuwa yanaweza kuzungumza Kinyarwanda (lugha ya Taifa). Hawa ndio ambao waliruhusiwa kuchukua bidhaa za Waarabu na za watu wengine wa nje ya nchi na kuziingiza nchini Rwanda au kutoa bidhaa nje ya nchi.

(c)       Wananchi wa Rwanda hawakuweza kuzungumza Kiswahili hasa hasa kwa vile hawakuweza kukutana kwa urahisi na watu wanaozungumza Kiswahili.

(d)       Kiswahili kimechelewa sana kuingia Rwanada. Inasadikiwa kuwa ni mnamo mwishoni mwa karne ya 19 tu ndipo Kiswahili kilianza kuingia nchini Rwanda kwa mara ya kwanza wakati wa utawala wa Kijerumani.

2   Sababu Zilizokieneza Kiswahili Nchini Rwanda Kabla ya Uhuru
Sababu kubwa zilizokieneza Kiswahili nchini Rwanda ni kama ifuatavyo:

(a)       Wajerumani waliwachukua baadhi ya watumishi kutoka Tanganyika, ambako idadi kubwa ya watu walikuwa wakizungumza Kiswahili na kuja nao Rwanda kufanya kazi.

Ni katika kipindi hicho ndipo Kiswahili kilianza kuingia nchini Rwanda na kuanza polepole kupata wazungumzaji.

 (b)      Mahubiri ya Dini Ya Ki-Islamu
Wengi wa watumishi kutoka Tanganyika ambao Wajerumani walikuja nao kufanya kazi Rwanda, walikuwa wakizungumza Kiswahil. Wengi wao walikuwa Waislamu. Wakati wa utawala wa Wajerumani Rwanda na Tanganyika, lugha ya mawasiliano ilikuwa ni Kiswahili katika shughuli za utawala.

Waislamu hawa pamoja na Waarabu walipokuwa wameshaipata nafasi ya kuingia Rwanda, wakaanza kuihubiri dini yao kwa lugha ya Kiswahili.

Baadhi ya Wanyarwanda walifuata Dini ya ki-Islamu na wakaanza kuelewa Kiswahili.

(c)       Mbeligiji ambaye ndiye aliyekuwa mtawala wa Rwanda baada ya kwisha Vita ya Pili (1945) na Mjerumani kuondoka Rwanda, hakukipenda Kiswahili; alikihusisha Kiswahili na uislamu ambao ni adui mkubwa wa wakristo wakiwemo Wabelgiji.

(d)       Shule

(i)        Shule ya Mfalme Yuki Musinga na Wasaidizi Wake
Kwa kuwa watawala wa jadi walipenda kuwasiliana na Wajerumani ambao walikuwa wanatumia Kiswahili katika shughuli zao, Mwaka 1900 Mfalme Yuki Musinga alikubali kufundishwa kwa mara ya kwanza yeye na wasaidizi wake lugha ya Kiswahili.

(ii)       Shule za Watawala wa Jadi
Kiswahili kiliruhusiwa kufundishwa katika shule za watawala wa jadi; na kwa hivyo kupewa nafasi ya kuena nchini Rwanda.

(iii)     Baada ya uhuru
Baada ya uhuru, Serikali iliona umuhimu wa kukiimarisha Kiswahili nchini Rwanda. Kwa hivyo, mwaka 1976/77 Kiswahili kikaanza tena kufundishwa katika Shule za Sekondari na katika Chuo Kikuu cha Rwanda. Nchini Rwanda, lugha ya Kiswahili ilifundishwa na walimu kutoka Tanzania.

(iv)      Juhudi za Wizara ya Elimu ya Taifa
Kutokana na mpango wa kufundisha Kiswahili katika shule za sekondari, Wizara ya Elimu ya Taifa ilianzisha kitengo cha kiswahili katika Taasisi ya Elimu ili kiweze kushughulikia vema ufundishaji na ukuaji wa Kiswahili.

Kazi ya kitengo cha kiswahili ni kutayarisha muhtasari, kuandika vitabu vya kufundishia, pamoja na ukaguzi wa Kiswahili katika shule za sekondari.

(v)       Redio Rwanda
Mnamo mwaka 1961 Redio Rwanda ilianza kutangaza baadhi ya vipindi kwa lugha ya Kiswahili. Vipindi hivi ni kama vile: ‘Taarifa ya Habari’, ‘Salamu za Wasikilizaji’, ‘Matangazo ya Mpira’, ‘Ulimwengu Tuishio, na vingine vya kuelimisha wananchi.

3       Matatizo Yaliyokabili Kuenea kwa Kiswahili Nchini Rwanda Baada ya Uhuru

Kwa uchache, matatizo husika ni:
 (a)      Uchache wa walimu – shule nyingine za sekondari hazikuwa na  walimu wa Kiswahili.

(b)       Kiburi cha Wanyarwanda -  Wananchi wa Rwanda walikuwa na kiburi, pengine mpaka leo; hawatilii maanani suala la kujifunza Kiswahili kwa sababu ya kuogopa kwamba Kinyarwanda,  lugha yao ya Taifa, ingemezwa na Kiswahili.

(c)       Wanyarwanda wanazihusudu sana lugha za Wazungu, hususan Kifaransa, Kiflemishi na Kiingereza kuliko lugha ya Kiafrika, hususan Kiswahili.                                
(d)       Uchache wa vitabu vya Kiswahili ulichangia na bado unachangia kwa kiasi kikubwa sana katika kupunguza kasi ya kuenea kwa Kiswahili nchini Rwanda.
Share on Google Plus

About Se

mwiza peter ni mwalimu ambaye alipata taaluma hii chuo cha ualimu morogoro(motco) kwa sasa nipo mwanza Tanzania ni miongoni mwa vijana ambao lengo langu nikukufanya wewe kupata elimu kuhusu somo la kiswahili na kuongeza ufaulu wa somo hili. tupo mwanza Tanzania.karibu mwaa tunawapenda wote.elimu ni ukombozi wa maisha chukua hatua
    Blogger Comment

0 comments:

Post a Comment